HECHE: MDEE, BULAYA NJOONI HADHARANI, MSITUME WATU


Kauli ya Mbunge John Heche baada ya kutishiwa maisha – Millardayo.com

VUGUVUGU la kuhoji uhalali wa ubunge wao tangu kufariki kwa Rais John Magufuli likiwa limepamba moto, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), John Heche amewataka wabunge 19 wa viti maalum waliokuwa wanachama wa chama hicho waliopo bungeni, kujitokeza hadharani kuomba radhi badala ya kuwatumia watu kuwaombea msamaha.

Heche ametoa kauli hiyo leo jana mjini Tarime, alipokuwa akizungumza na wanachama wa Chadema katika mkutano wao wa ndani.

Amesema wamepata taarifa kutoka kwa baadhi ya watu ambao wametumwa na wabunge hao kuwaombea msamaha, jambo ambalo halikubaliki.

Akifafanua, alisema wabunge hao wanapaswa kutambua kuwa chama hicho sio timu ya mpira wala bendi ya kutoa burudani, isipokuwa kina nia ya kubadilisha maisha ya Watanzania kutoka katika umasikini na kuishi maisha mazuri kulingana na rasilimali zilizopo.

“Hawa wasituletee maigizo hapa na watambue kuwa hawana umaarufu kuliko watu kama kina Zitto Kabwe na Dk. Slaa ambao baada ya kuona wanataka kutuzamisha tuliwatosa sisi tukasonga mbele,” amesema Heche.

Amesema kama yupo mbunge mwenye nia ya kuendelea kuwa mwanachama wa chama hicho, ajitokeze hadharani aombe radhi ili wanachama na uongozi uweze kupima kama anastahili kusamehewa ama la.

Amesema Chadema hakijasahau usaliti uliofanywa na wao ambao walishuhudia mateso waliyoyapata hasa wakati wa uchaguzi, ambapo baadhi ya watu walipoteza maisha mbele zao lakini walipoambiwa chama hakikubaliani na matokeo ya uchaguzi, wao walijitenga na kuwasaliti.

“ Hawa ndugu zetu walishuhudia magumu tuliyopitia, mfano mimi siku ya kufunga kampeni pale Nyamongo, kuna watu walipoteza maisha baada ya mkutano wangu kuvamiwa na polisi na kuanza kurusha risasi hovyo na haya yote hawa wenzetu wanayajua kwa undani. Kwa sababu walikuwa ni wajumbe wa kamati kuu lakini waliamua kuangalia maslahi yao binafsi na kuwasahau watu waliojeruhiwa, wengine kupoteza maisha kwa sababu yao,” amesema Heche.

Amesema Chadema bado haijabadilisha dhamira yake ya kubadili maisha ya watu kutoka hali ya unyonge na umasikini, ambayo inatumiwa na wapinzani wao kuendelea kuwatawala Watanzania.

Amesema nia hiyo itafanikiwa kwa kutumia rasilimali zilizopo endapo tu chama kitapata ridhaa ya kuongoza dola.

 

No comments