SITA WAHOFIA KUFA MAJI MTO RUVUMA WILAYANI NYASA
![]()
Na Stephano Mango, Nyasa
WATU sita wa familia mbili wakazi wa kijiji cha Mipotopoto, kata
ya mitomoni Wilaya Nyasa mkoani Ruvuma wanahofiwa kufa maji baada ya mtumbwi
(gome) waliokuwa wakisafiria kutoka kijijini hapo kwenda mashambani ambayo yapo
ng’ambo ya mto Ruvuma kuzidiwa uzito na kuzama.
Akizungumza na gazeti hili jana Kaimu Kamanda wa Jeshi la Zima
moto na Uokoaji Mkoani Ruvuma Mkaguzi Msaidizi Chesco Mbata alisema kuwa tukio
hilo limetokea Mei 22 mwaka huu majira ya saa 12 asubuhi huko eneo la mto
Ruvuma na kusababisha maafa hayo.
Kaimu Kamanda Mbata aliwataja watu hao ambao wanahofia kufa maji
kuwa ni Yusuph Ummy (28) Fitina Salum(22) Fahim Ummy (2) Tosha Salum
Kalomba(30) Emran Mohamed Chiponda(1) na Rambo Mohamed Chiponda(6)
Alisema kuwa inadaiwa siku hiyo ya tukio watu hao wa familia
mbili walikuwa wakitokea nyumbani kwao na kwenda katika shughuli zao
za kilimo kwa kutumia usafiri wa kienyeji wa mtumbwi maarufu kwa jina la gome
na kwamba walipofika katikati ya mto mtumbwi ulizidiwa na kasi ya mawimbi ya
maji na kusababisha mtumbwi huo kupoteza muelekeo na kuzama majini.
Alifafanua zaidi kuwa baada ya kupokea taarifa hizo kutoka
katika uongozi wa kijiji cha Mitomoni kupitia Jeshi la Polisi Wilayani Nyasa,
askari wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa kushirikiana na Kamati ya Ulinzi na
Usalama ngazi ya Wilaya na Mkoa walifika eneo la tukio ambako waliwakuta wananchi
wakiendelea kuwatafuta watu hao waliozama.
Alisema kuwa katika juhudi za uokoaji mtu mmoja ambaye
amefahamika kwa jina la Emran Mohamed Chiponda(1) alipatikana na kukimbizwa
katika Kituo cha Afya cha Liparamba ambako baadae alifariki dunia wakati
anaendelea kupatiwa matibabu.
Mkuu wa Wilaya ya Nyasa Isabela Chilumba alipohojiwa na blog
hii, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kutoa wito kwa wananchi ambao
wanazunguka ziwa Nyasa na mito mikubwa yote iliyopo wilayani humo kuchukua tahadhari wanapovuka
mito hiyo kwani imekuwa na mawimbi na kasi kubwa ya maji.
Kwa Upande wake kamanda wa Polisi Mkoa wa Ruvuma Simon Maigwa alisema
kuwa jitihada za uokoaji zinaendelea na kutoa wito kwa wananchi kuacha kutumia
chelezo aina ya gome katika kuvuka mito mikubwa kwa usalama wa maisha yao.

Post a Comment