MBUNGE CATHERINE MAGIGE KUADHIBIWA NA CCM

KUFUATIA kitendo chake kisicho cha
kimaadili cha kwenda kuleta vurugu katika msiba wa mtu anayemtaja kama mchumba
wake, Chama cha Mapinduzi (CCM) kimechukizwa na kulaani kitendo alichofanya
Mbunge wake, Catherine Magige na kuahidi kumchukulia hatua.
Mbunge huyo jana Alhamisi Mei 27, 2021 alikwenda makaburini
yalikokuwa yakifanyika mazishi ya mfanyabiashara Kuzula Madoda inayedaiwa kuwa
ni mchumba wake. Madoda alifariki dunia Mei 24, 2021 na ameacha mke, Aziza
Msuya na watoto.
Kitendo cha Catherine kwenda makaburini kiliibua hali ya
sintofahamu kutokana na watu waliokuwa naye kuvunja geti na kuingia katika
makaburi hayo ya familia.
Taarifa ya chama hicho iliyotolewa na katibu wa itikadi na
uenezi, Shaka Hamdu Shaka leo Ijumaa Mei 28,2021 inaeleza kuwa CCM inaheshimu
katika kujenga uimara wa familia, kuheshimiana ndani ya jamii na kuendeleza
upendo katika familia halali badala ya mivutano na uvurugaji usiokuwa na sababu.
"Chama kinatafakari kwa undani kwa mujibu wa kanuni za
maadili na katiba ya CCM na kuchunguza kwa kina ili kuchukua hatua za kimaadili
kwa wote watakaothibitika kuwa sehemu ya matukio yaliyojenga kukiuka kwa
katiba, kanuni na utamaduni wa kuheshimu na kuheshimiana uliojengeka ndani ya
CCM," inaeleza taarifa hiyo.

Post a Comment