KUWA MUAMINIFU, ILA USIMUAMINI MTU


Mtu mwaminifu ni nani? Kwa nini Mungu huwapenda watu waaminifu? – Mwenyezi  Mungu-Kurudi kwa Bwana Yesu

KUNA utofauti kati ya kuwa mwaminifu na kumwamini mtu. Mtu muaminifu ni yule anayefanya yale yampasayo kufanya pasipo udanganyifu au hila yenye nia ofu.

Akipewa kapu lenye maembe mia moja alipeleke sehemu, atalifikisha kama lilivyo, bila kula embe hata moja njiani kisha huko aendako, adanganye moja lilioza. Huyu ni mtu muaminifu.

Kumuamini mtu ni kitendo chako cha kuwa na imani na mtu kwa asilimia mia moja. Yaani, kila jambo lako, hausiti kumshirikisha kwa kuamini kuwa atakuhifadhi na kukusitiri, iwe jua, iwe mvua!

Nadhani hapo nitakuwa nimeeleweka. Wakati flani nilikuwa nafanya kazi kwa bosi wangu mmoja hivi, nikisimamia mashine za kamari ambazo siku hizi zimewekwa baa, ambazo zinaitwa Slots Machine.

Mmoja kati ya wachezaji wakubwa wa kamari zile, alikuwa ni mzee mmoja hivi ambaye baadaye tulikuja kuwa marafiki sana. Hapo kabla yangu, kulikuwa na msimamizi mwingine ambaye kuna mambo walikuwa wanayafanya, kila mmoja akinufaika, sikuwahi kuyaelewa.

Yule mtangulizi wangu alipokuja kuondoka na kuwekwa mimi, mzee yule akawa hanielewi, lakini akawa anakuja taratibu kutaka ukaribu. Na kwa kuwa alikuwa ni mteja mzuri, nami nikajisogeza, tukawa maswahiba!

Siku moja akanialika nyumbani kwake baada ya saa za kazi. Haikuwa mbali na kazini kwangu, so nikaenda. Nilimkuta na familia yake, mkewe na watoto wengine ambao tulilingana umri na kumbe tulifahamiana pia.

Tukiwa peke yetu, yule mzee akanipa mchongo ambao ulihusu pale kazini kwangu. Kwamba kama ningefanya hivi, kwa pamoja tungeweza kupata kiasi kikubwa cha pesa. Yaani ilikuwa hivi; hizi mashine zikichezwa sana, coin zile, yaani hizi sarafu zinazotumbukizwa, hujaa.

Kwa kuwa zamani mashine hizi ziliwekwa katika vyumba, siyo baa kama hivi sasa, wakati wa kuzitoa hizi sarafu, huja wafanyakazi maalum kutoka ile ofisi mnafanya nayo kazi, enzi hizo sisi tukifanya kazi na Las Vegas Casino. Wakija mnafunga milango ili zoezi la kutoa sarafu lifanyike!

Kwa mfano wakati ule tulikuwa na mashine kama sita hivi, ambazo wakija kutoa coin zilizojaa, wangeweza kutoa hadi za milioni moja na ushee.

Kulikuwa na mchezo unachezwa. Wale wafanyakazi wa casino, walikuwa wanamtumia yule mzee, kutushawishi, kwamba wakati wa kutoa zile sarafu, kama ni za milioni moja kwa mfano, kule Casino wapeleke labda laki saba, hizi tatu tugawane. Huu ni mchezo wa kila wiki, just imagine hii ni katikati mwa 1990!

Mimi nikakataa. Nikasema siwezi kwa sababu kubwa mbili, kwanza ni mgeni pale kazini, halafu pia siwezi kumuamini yeye, yaani yule mzee. Akaniambia hiyo sababu ya kwanza nimeielewa, ya pili, huniamini kwa nini?

Nikamwambia nitajuaje kama hajatumwa na mabosi wangu kunichunguza? Ajabu, badala ya kukasirika na uhusiano wetu kuanza kuzorota, ndiyo kwanza ukashamiri na hakuwahi tena kuniambia habari zile ila aliniambiaga sentensi moja kwamba Uaminifu Unalipa!

Yeah, huo ni mfano unaonihusu. Katika maisha yetu ya kila siku, haya mambo tunakutana nayo. Uaminifu, wengine wanasema ni mtaji. Ukijitahidi ukawa muaminifu leo, kesho unaweza kukupatia kazi, maisha, rafiki au hata jambo ambalo hukulitegemea.

Uaminifu ni ile hali ya kuridhika na hali yako na kuibana nafsi iache tamaa. Uaminifu si katika fedha tu, hata katika maisha ya kawaida mitaani. Mtu kakukaribisha nyumbani kwake, unaishi naye kama ndugu, acha tamaa ya kingono ya kumtamani mwanaye, mkewe au ndugu yeyote pale!

Umepata kibarua, unalipwa kidogo, lakini kuna vitu ukivichukua, huku mtaani unapata hela zaidi. Achana na hizo tamaa, mwenye mali anajua kuna nini pale alipokuweka, anapima imani yako tu. Ukikomaa na kazi yako na usiguse kisichokuhusu, huyu mtu anatafuta mtu wa namna yako, huwezi jua kuna sehemu bora zaidi anahitaji kukuweka, vitu vingine huwa ni mitego tunawekewa na sisi tunanasa kirahisi.

Hii ni mifano michache, lakini ninaamini unafahamu ninapojaribu kwenda, kwamba popote ulipo, jitahidi kuizuia nafsi yako isitamani kisicho chako, ukibanwa sana, omba!

Lakini pia moja kati ya maeneo tunayokosea sana, ni kuwaamini watu ovyo ovyo. Mmekutana tu huko kibaruani, mara eti kawa mtu wako wa karibu, no, no, no, tena big no!

Trust nobody my bra. Achana na huyo mtu mmekutana kibaruani, usimuamini hata mkeo/mumeo. Hapa usinielewe vibaya, kuna kuamini na kupenda. Mpende mkeo/mumeo, lakini usimuamini 100%.

You know what? Watu waovu katika maisha yako, hupitia kwa unayemuamini. Wakishaona wewe na flani ni maswahiba wa kushibana, hupitia kule. Sasa kama huyo swahiba wako umemuachia mlango wazi, anajua kila kilichomo ndani mwako, anajua unapoweka silaha, anajua udhaifu wako, anajua unachokitegemea, kuna nini tena hapo?

Usiruhusu hili jambo litokee. Hata mke/mume wako kuna mambo hapaswi kujua kwa sababu nani anajua kuwa kesho mnaweza mkawa maadui? Kuna baadhi ya silaha ni zako peke yako, utazitumia pale mtu wako wa karibu atakapotaka kuwa tishio, maana hatajua kama unazo.

Ishu siyo kukorofishana na mtu wako wa karibu, ujumbe hapa ni kwamba usiyaanike maisha yako kwa mtu mwingine ye yote, jitahidi kadiri unavyoweza, mambo yako ya msingi yabaki kuwa ya kwako. Binadamu, hasa sisi ngozi nyeusi hatupendani, leo utajianika kwa huyo unayedhani rafiki yako, kesho mtaa mzima wanajua ulivyo. Unatembea uko uchi, mwenyewe unajiona umevaa nguo!

 

 

 

 

No comments