JACQUELINE NTUYABALIWE ANA LAKE JAMBO

 

Inaweza kuwa picha ya Watu 4, watu wanasimama na maandishi yanayosema 'Jacqueline N Mengi 21h I bet those who have read the| CAN I MUST I WILL will be very surprised to hear that someone out there has declared the author of the book @regmengi to have been mentally unsound when he wrote and launched that book. This world will never cease to amaze me!'

JACQUELINE Ntuyabaliwe, aliyekuwa mke wa pili wa Marehemu Reginald Mengi amesema mumewe hakuwa na matatizo ya akili kama inavyodaiwa  na kuwataka wanaotoa  madai hayo kuacha uzushi.

Ameeleza hayo kupitia ukurasa wake katika mtandao wa kijamii wa Twitter, ikiwa zimepita siku tatu tangu Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kuukataa wosia uliokuwa ukidaiwa kuandikwa na Mengi ambaye alikuwa mfanyabiashara maarufu nchini ambapo pamoja na mambo mengine ikieleza kuwa haukidhi matakwa ya kisheria ili kuwa wosia halali.

Katika maelezo yake aliyoyatoa jana Alhamisi Mei 20, 2021 mlimbwende huyo wa Tanzania mwaka 2000 amesema wanaoibua uzushi huo wanaweza kusema chochote wanachojisikia na kuchukua mali zote lakini hawezi akakaa kimya na kuacha wamchafue Mengi, atasimama na kumtetea katika hilo.

“Hii ni ripoti yake ya hospitali, huu ni kweli kwa wale ambao wanataka kupata uhakika. Mume wangu hakuwa na matatizo ya kiakili.”

“Mnaweza mkasema chochote mnachojisikia na kuchukua kila kitu lakini kwa hili nitamtetea hadi umauti wangu utakaponifika. Daktari Kaushik Ranchod kutoka Afrika Kusini na daktari Anthony Rudd kutoka Uingereza wanaujua ukweli kuhusu hili,” amesema Jacqueline aliyeambatanisha picha ya ripoti ya hospitali ya Mengi aliyefariki dunia Mei 2, 2019.

Uamuzi wa Mahakama Kuu ulitolewa Jumanne Mei 18, 2021 na Jaji Yose Mlyambina kufuatia shauri la mirathi lililokuwa limefunguliwa na watu wanne wakiwemo ndugu wa marehemu, wakiomba kuteuliwa kuwa wasimamizi wa mirathi hiyo.

Jaji Mlyambina amefikia uamuzi huo baada ya kukubaliana na hoja za pingamizi lililowekwa na mmoja wa watoto wakubwa wa marehemu Mengi pamoja na ndugu yake marehemu Mengi, waliokuwa wakipinga uhalali wa wosia huo ambao pamoja na mambo mengine uliandikwa kuwa watoto wakubwa wa Marehemu wasipewe chochote katika mali za Marehemu na kama wataenda Mahakamani kupinga wosia huo wakishinda kesi wapewe shilingi elfu moja tu (Tsh 1000/=) katika mali za Marehemu Baba yao.

Shauri hilo la mirathi namba 39 la mwaka 2019 lilifunguliwa na Benson Benjamin Mengi, William Onesmo Mushi, Zoebu Hassuji na Sylvia Novatus Mushi wakiomba kuteuliwa kuwa wasimamizi mirathi hiyo kwa mujibu wa wosia huo.

Hata hivyo, mtoto wa marehemu Mengi, Abdiel Reginald Mengi na ndugu wa Mengi, Benjamin Abraham Mengi, waliweka pingamizi dhidi ya wosia huo, wakipinga uhalali wake huku wakiwasilisha jumla ya sababu nne za kuupinga.

Sababu hizo ni pamoja na kwamba haukwa umepigwa mhuri na saini iliyokuwepo ilikuwa ni tofauti na saini ya kawaida ya marehemu Mengi na kwamba haukushuhudiwa na ndugu au mke wa marehemu.

Pia walikuwa wakidai kuwa marehemu hakuwa na uwezo wa kuandaa wosia kwa kuwa alikuwa na matatizo ya kiafya tangu mwaka 2016 na kwamba unaondoa katika urithi, watoto bila kuzingatia mila za Kichaga au kuhusisha ndugu.

Mahakama Kuu baada ya kusikiliza hoja za pande zote katika hukumu yake iliyosomwa na Jaji Mlyambina na nakala yake kupatikana kwa matumizi ya umma, alikubaliana na hoja za pingamizi hilo dhidi ya wosia huo na kuikataa kuwa ni batili.

Jaji Mlyambina alikubaliana na sababu hizo za pingamizi na pamoja na mambo mengine, amesema kuwa inawanyima urithi wanaye bila kutoa sababu, na kwamba ziliiingizwa mali za mke wake mkubwa.

Kwa uamuzi huo, Jaji Mlyambina hakuwateua waombaji hao kuwa wasimamizi wa mirathi na badala yake aliwateua Abdiel na Benjamini kuwa wasimamizi wa mirathi na akaelekeza mali za marehemu zigawiwe warithi wanaostahili kwa utaratibu wa kawaida kama wa mtu ambaye hakuacha wosia.

Awali mjane wa marehemu Mengi, Jacquiline alijaribu kuingia katika shauri hilo bila mafanikio baada ya mahakama hiyo kutupilia mbali maombi yake mara tatu.

 

No comments