UKINIZINGUA TUTAZINGUANA
NI kauli ya Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan 'Sasha' wakati akitoa
nasaha zake baada ya kuwaapisha Makatibu Wakuu wa Wizara na Manaibu wao, Wakuu
wa Taasisi za serikali na viongozi wengine kwa ujumla, Ikulu jijini Dar es
Salaam.
Ghafla, umekuwa
msemo mkubwa, maarufu na unaotumiwa na wengi kama kibwagizo, huku dalili za
awali zikionyesha watu wengi wanamuunga mkono rais huyo wa kwanza mwanamke hapa
nchini.
Katika kipindi
kifupi tangu akabidhiwe ofisi kufuatia kifo cha Rais wa Awamu ya Tano, John
Pombe Magufuli aliyetangazwa kufariki Machi 17, 2021, Madame Sasha amezungumza
mambo mengi yanayotoa ishara ya kurekebisha baadhi ya vitu ambavyo vilifanyika enzi za mtangulizi wake.
Vitu hivyo ni kama
ubabe uliokuwa ukitumika wakati wa ukusanyaji kodi, akiagiza weledi kutumika
zaidi, ili kuweka mazingira ya kuwavutia na kuwatengeneza walipa kodi wapya na
kuwazuia waliopo kufunga au kuhamisha biashara zao.
Mama Samia pia
ametaka haki kutendeka, amekataza dhuluma na kubambikia watu kesi za chuki na
visasi. Kumekuwa na kelele kutoka kwa baadhi ya watu wakidai maofisa wa
serikali kutumia mamlaka yao kuwapa kesi ambazo hazina ushahidi, kama vile
uhujumu uchumi.
Aliwaagiza maofisa
wa serikali kuzifuta kesi zote zinazoidhalilisha kwani zinapelekwa mahakamani,
lakini zinashindwa. Jambo hili lilipokewa kwa faraja na matumaini.
Ndani ya kipindi
kisichozidi mwezi mmoja, Rais Samia Suluhu Hassan, pia amefanya mabadiliko
katika taasisi za serikali na kutoa maagizo. Kwanza alimsimamisha kazi
aliyekuwa Mkurugenzi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania na kuiagiza Taasisi ya
Kuzuia na Kupambana na Rushwa kufanya uchunguzi wa upotevu wa mabilioni ya
shilingi ndani ya taasisi hiyo.
Wakati wa utawala
wa mtangulizi wake, vyombo vingi vya habari, hasa magazeti vilifungiwa na
vingine kufutwa kwa sababu mbalimbali. Ameagiza kufunguliwa kwa vyombo hivyo
ili kuonyesha uhuru wa kujieleza, lakini akielekeza vyombo hivyo kuelekezwa
kanuni.
Magazeti kama MwanaHalisi,
Tanzania Daima, Mawio na mengineyo, ambayo yaliandika habari za ubadhilifu wa
wanasiasa, wafanyabiashara na wakati mwingine kukosoa utawala, yalifungiwa na
mengine kufutwa kabisa kwa sababu mbalimbali.
Licha ya magazeti
hayo, lakini pia waandishi wengi wa habari walioandika kuhusu ubadhilifu wa
mali za umma, wengi walipatwa na madhira mbalimbali, ikiwa ni pamoja na kupewa
kesi za uhujumu uchumi.
Pia sambamba na
hiyo, sheria kadhaa zilitungwa zikilenga kuwadhibiti magazeti na waandishi.

Post a Comment