Simba inakuzwa au inastahili?

Hakuna ubishi kwamba kwa sasa, Simba inacheza
soka safi la kuvutia, mashabiki wake wakiubatiza kuwa ni soka biriyani.
Siyo tu inacheza vizuri, lakini pia timu hiyo
ina lundo la wachezaji wenye vipaji. Lakini katikati ya ukweli huo, kuna baadhi
ya mashabiki wanahisi wekundu hao wa Msimbazi wanakuzwa.
Kwamba ni timu ya kawaida kabisa, kama zilivyo
zingine za Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu. Wanaifananisha na Kagera Sugar,
Mtibwa, Prisons, Mbeya City, KMC, Biashara, Mwadui, Dodoma Jiji, Polisi
Tanzania, JKT Tanzania na Namungo.
Je ni kweli mawazo haya yako sawa?
Lolote linaweza kuwa jibu sahihi kutegemea na
nini mwandishi atazungumzia. Kwangu mimi nitajaribu kueleza ni kwa nini
ninaamini ninavyoamini.
Kimichezo, Simba iko sawa na timu hizo zote
pamoja na Yanga na Azam FC, kwani zote zinacheza ligi moja ambayo hutoa bingwa
wa nchi anayewakilisha katika michuano ya kimataifa inayohusisha timu zingine
mabingwa barani Afrika.
Lakini kama tutazungumza kuhusu viwango vya
soka, siyo sawa kuzifananisha timu hizo na Simba, kwa kuwa kiwango chake, licha
ya kucheza ligi moja, lakini ni kikubwa.
Karibu asilimia 95 za mecho zote 19 ambazo Simba
imecheza hadi sasa, imeongoza kwa kumiliki mpira (ball possession) licha ya
kuwa imefungwa mechi mbili na sare tatu.
Ingawa kuna timu zimeshacheza mechi 23 za Ligi
Kuu, nne zaidi yake, Simba ndiyo timu iliyofunga mabao mengi (45) na ndiyo
iliyofungwa mabao machache zaidi (8). Maana yake ni nini?
Kwamba Simba ndiyo timu yenye washambuliaji
hatari zaidi ya timu zote, ikiwa pia ndiyo timu yenye ukuta mgumu zaidi. Kwa
tafsiri nyingine, ndicho kikosi chenye safu bora zaidi ya kiungo, kinachofanya
kazi nzuri ya kuunganisha mabeki na washambuliaji.
Huu ni ubingwa wa tatu mfululizo wa nchi,
ikiufukuza ubingwa wa nne msimu huu. Yanga, yenye michezo 23 tayari dimbani,
inaongoza ligi ikiwa na pointi 50, tano mbele ya Simba, ambayo ina mechi nne
mkononi.
Endapo Simba itashinda mechi hizo (Uwezekano huo
upo) itafikisha pointi 57, ikimaanisha itawaacha Wananchi kwa pointi saba.
Kuthibitisha ubora wa kikosi hicho chini ya
kocha wao Mfaransa Didier Gomez Da Rosa, Simba inaongoza katika kundi lao
kwenye ligi ya mabingwa barani Afrika, ambako kabla ya kuanza, iliwekwa nafasi
ya nne na ya mwisho kwa ubora.
Imekuwa klabu ya kwanza kutoka Tanzania kupata
pointi nne ugenini katika michuano hiyo, ikishinda nyumbani kwa AS Vita kule
Kinshasa na baadaye kuitunishia misuli El Merreikh jijini Khartoum, hiyo ikiwa
ni pamoja na kuwapiga mabingwa watetezi wa Afrika, Al Ahyl, mchezo uliofanyika
Uwanja wa Benjamin Mkapa.
Na katika michezo hiyo yote, kiwango cha Simba
kilikuwa juu kuliko timu hizo zote. Wanaonekana wakicheza kwa uelewano mkubwa
na kujiamini, bila kujali kama wanacheza nyumbani au ugenini.
Na kwa mara nyingine tena, Simba inakuwa timu ya
kwanza kuwapa imani watanzania kuwa itafuzu hatua za makundi msimu huu ikiwa
kinara. Wapo wanaoamini pia kuwa timu hii inao uwezo wa kuingia fainali na hata
kutwaa taji hilo.
Haya ni mambo ambayo yanaleta utofauti mkubwa
kati ya Simba na timu zingine zinazoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara. Licha ya
kucheza ligi moja, lakini siyo timu zote hizo zinaweza kuifunga Al Ahyl
nyumbani.
Kama kuna mtu anaikuza Simba, anayo sababu ya
msingi ya kufanya hivyo na kama yupo anayeishusha, ni kutegemea tu na kwamba
anataka kuifananisha na timu zipi, lakini ni kama hizi za ligi kuu, anaweza
kuwa ana sababu binafsi zisizo za kimchezo.

Post a Comment