Jiepushe na mambo haya kipindi hiki
Hivi sasa kila mmoja analalamika juu ya hali
ngumu ya maisha. Na mambo ni magumu kweli ndugu zangu, ingawa katikati ya msoto
huu, wapo ambao wanakula raha hadi wanaboa.
Si mfanyabiashara, si mfanyakazi, si mkulima, si
mjasiriamali, kilio ni kilekile, hali mbaya, hamna hela. Miaka michache iliyopita, ungeweza kukusanya
hadi laki tano kwa mwezi kwa 'mizinga' tu, lakini sasa hivi, thubutu, ukipata
hata laki shukuru.
Na mizinga hiyo siyo kwamba ulikuwa unawapiga
watu wasiwasi, la hasha. Ni watu wako wa karibu ambao wana kazi za kawaida tu
huko makazini mwao, wafanyabiashara wa kiwango cha kati tu na hata
wajasiriamali.
Lakini sasa hivi kila mmoja anakwambia vyuma
vimekaza. Na ushahidi kwamba vyuma vimekaza wala hauhitaji upelelezi wa ofisa
wa polisi aliyekubuhu. Unaona tu mwenyewe kwa macho ya kawaida.
Kulikuwa na mabosi wana gari nne hadi tano uani
mwao na yote yako barabarani. Moja la mzee, moja la mama, lingine la kusombea
vyakula vya mifugo kama ng'ombe, mbuzi na kuku, gari jingine la kuwapeleka na
kuwarudisha watoto shuleni na lingine
lipolipo tu attention, lakini liko full tanki.
Sasa hivi unaona, magari matatu yameuzwa,
yamebaki mawili, moja la kusombea vyakula vya mifugo la lingine wanatumia wote
baba na mama kwenda na kurudi kazini.
Wapo baadhi, hawana hata gari moja. Zamani kila
siku kwao ilikuwa sherehe, sasa hivi kukiwa na shughuli majirani wanajiuliza
kunani pale?
Huu ni ushahidi kuwa hali ni ngumu kwelikweli na
haya yafuatayo ni baadhi ya mambo ambayo ni vyema ukajiepusha nayo kwa sababu
yanaweza kukufanya ukajikuta uko katika wakati ambao haukuutarajia.
1.
Hasira
Punguza sana tabia ya kuwa mtu wa hasira hasira,
unayekasirika bila sababu za msingi. Jambo dogo tu umepandisha mori, utajikuta
umefanya jambo ambalo litakugharimu.
Kumbuka, ni nadra kufanya maamuzi ya busara
ukiwa na hasira. Rafiki mkubwa wa hasira ni matusi, ugomvi na mambo mengine
yanayoambatana na ukosefu wa staha.
Katika nyakati hizi ngumu kimaisha, watu
hawakawii kutumia udhaifu wa hasira zako kujinufaisha na ulichokifanya
ulipokuwa na hizo hasira zako.
Watu watakupeleka polisi, serikali ya mtaa au
hata kwa mjumbe wa nyumba kumi, ambako utajikuta ukilazimika kuingia mfukoni
kwa jambo ambalo ungeweza kulishinda kwa kumezea tu.
Kuna watu wana maisha angalau kidogo ni mazuri,
lakini wana hasira. Inapotokea hivyo wana kawaida ya kutoa maneno ya shombo,
matusi au hata kurusha ngumi. Ni vyema ukatambua kwamba maneno ya kejeli kwa
mwenzako, matusi au kumpiga, vyote ni kinyume cha sheria na unaweza kuadhibiwa
hadi kifungo.
Kuna watu wanakuonea wivu na maisha yako lakini
hawajui watakupataje. Wengine wanasubiri ujihukumu kwa udhaifu wako.
2.
Jifunze kuwa peke yako
Nyakati hizi ni ngumu hivyo ina mambo mengi.
Wapo baadhi yetu tuna kawaida ya kupitia labda baa kupata moja mbili kabla ya
kurejea nyumbani. Katika kipindi hiki, ni vyema ukajifunza kuwa peke yako, hata
kama ni baa.
Hii haimaanishi kuwa hautaki ushirikiano na
wenzako, la hasha. Wape hi washkaji ukiwakuta, kisha sogea pembeni kwa sababu
zozote, kama vile kuna simu muhimu naisubiri na kadhalika.
Hiyo ni kama ni lazima uende bar, lakini kama
ishu ni kunywa, chukua vinywaji nenda kanywee nyumbani. Mwingine anaweza kusema
hawezi kubeba bia kumi, fine, kuna bar karibu na unapoishi.
Ukifika mtume kijana akuchukulie bia zako nywea
nyumbani kwako. Hii siyo tu itakupunguzia wadowezi, lakini itakuepusha na mambo
mengi.
Nitakupa mfano halisi. Jamaa yangu mmoja
alijikuta akikabiliwa na tuhuma ambazo hakuwahi kujua zilikotokea. Alitoka
katika mihangaiko yake akafikia baa akisema apoze koo kidogo. Mara wakatokea
vijana wawili na kujiunga naye.
Kwanza walimuagizia anachokunywa na baadaye
akawanunulia nao pia. Wakajikuta wamekuwa marafiki kiasi cha hata kugongesheana
mikono katika maongezi.
Ghafla wakatokea watu waliojitambulisha kama
askari, wakawaambia wako chini ya ulinzi. Wakabebwa hadi kituo kimoja kidogo
cha polisi ambako wale jamaa wawili walikiri kuwa ni wahalifu na kwamba huyo
jamaa ni mwenzao!
Ule ulikuwa ni mchongo wa polisi na wale vijana,
ikabidi jamaa yangu atoe fedha nyingi kunusuru mashtaka ambayo yangeweza
kumpotezea gerezani. Mifano ipo mingi. Watu wanaweza kukujumuisha kwenye genge
la uhalifu bila wewe kujua kuwa ulikuwa ni mchongo, lakini ukiwa na tabia ya
kutojichanganya, unaweza kuepuka baadhi ya mambo.

Post a Comment