SAFARI YA MWISHO KABISA YA MAGUFULI

 

RAIS wa awamu ya Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Magufuli, leo atafanya safari ya mwisho kabisa duniani, wakati mwili wake utakapowasili kijiji alichozaliwa cha Chato, mkoani Geita.

Safari hiyo ilianzia katika Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza ambako msafara wa magari uliondoka, baada ya kuagwa na umati wa maelfu kwa maelfu ya wananchi waliojitokeza kutoa heshima zao za mwisho.

Magufuli, aliyepachikwa majina mengi ya utani kama vile Jiwe, Mwamba na Jeshi, alitangazwa kufariki Machi 17 mwaka huu, kwa maradhi ya moyo.

Kabla ya safari yake ya mwisho hapo jana, aliagwa kwa siku mbili mfululizo jijini Dar es Salaam, siku moja Makao Makuu ya Nchi, Dodoma, siku moja pia katika sehemu ya pili ya Muungano, huko Zanzibar.

Magufuli anakuwa rais wa kwanza wa Tanzania kufariki akiwa madarakani, rekodi ambayo imeandika rekodi nyingine ya kupata mwanamke wa kwanza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ambaye aliapishwa kuchukua nafasi hiyo kwa matakwa ya katiba. 

No comments