Kufungwa WhatsApp kwawavuruga watu

 


KUSUDIO la serikali kuthibiti matumizi ya mtandao wa WhatsApp limepokelewa kwa hisia tofauti, huku wananchi wengi wakivurugwa, kwani hawaelewi nini hasa lengo la jambo hilo.

Siku chache zilizopita, Waziri wa Habari na Teknolojia, Faustine Ndungulile alisema matumizi ya mtandao huo katika video calls, simu za kawaida na sms, yamekuwa yakichangia kwa kiwango kikubwa kuporomoka kwa mapato kwa makampuni ya simu na mapato ya serikali.

Hivyo, wanataraji kudhibiti matumizi hayo ili kuwafanya watumiaji hao kuchangia gharama hizo, jambo linalopigwa na wadau wakidai juhudi hizo ni kupingana na ukuaji wa teknolojia, jambo ambalo halitafanikiwa.

"Serikali haiwezi kushindana na ukuaji wa teknolojia, badala ya kutafuta njia za kupambana nayo, ni vyema iangalie namna ya kukabiliana nayo kwa ubunifu wa namna nyingine ya wao kuweza kupata mapato," anasema mwanafunzi mmoja wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam aliyejitambulisha kwa jina moja na Vivian.

"Teknolojia inakuja kwa ajili ya kurahisisha maisha, sasa wewe unakataa unataka watu bado waendelee kuishi kizamani, kweli?" alihoji mwananchi mwingine aliyefikiwa na Batablogspot.com.

"Mimi nimekuwa nikifanya biashara na kupata wateja wangu kutoka mbali na nilipo kwa kuongeo na kuwaonyesha bidhaa zangu kupitia video call, hii imenirahisishia maisha. Sasa serikali gani ya wanyonge inataka watu waendelee kutaabika wakati teknolojia inawasaidia?

"Cha msingi wao wakae na kubuni namna ya kukabiliana na changamoto hii. Makampuni ya simu yapunguze gharama za vifurushi wateja wataongezeka na serikali itapata mapato. Yaani serikali inataka kuyasaidia makampuni ya simu kwa gharama za wanyonge?"

 

No comments