CHOZI LA BINTI KIMITI KWA JPM TOKA UGHAIBUNI
KIFO
hakizoeleki ingawa kipo na tunaishi nacho, kila uchwao kimekuwa kikichukua
wazazi wetu, watoto wetu, dada, kaka, jamaa, rafiki na hata jirani zetu.
Kama kifo
kingeweza kuonekana, naamini hakuna mtu angekubali kukutana nacho. Hata
walemavu wa miguu wangekikimbia.
Kifo ni fumbo
la imani ambalo halijapata wa kulifumbua tangu dunia iumbwe.
Ugumu wa
kukiona kifo umekuwa mtihani hata kwa majemedari na mashujaa wa kijeshi.
Ushujaa wao unakuwa ni udhaifu mbele ya kifo.
Ubaya wa kifo
ni kutokuchagua, kifo kinachukua wema na wabaya, wakubwa na hata wadogo.
Kifo sasa
kinailiza dunia, kifo kimemchukua shujaa wa Tanzania, mpambanaji na jemedari wa
kweli Dk. John Pombe Magufuli.
Dk. Magufuli
sasa ni hayati, mwili wake umo ndani ya jeneza, amelala, amelala milele na
hawezi kupumua tena.
Kwa sasa kaburi
ndio makazi yake, hawezi kusimama tena na kuwakemea mafisadi na wadhalimu
waliokuwa wakipoka haki za wanyonge.
Mwangi wa vilio
vya Watanzania, Waafrika na dunia kwa ujumla, unaelekea kwenye jeneza lake.
Watu wanalia,
wanamkumbuka, hakuna anayeamini kama mwamba umeanguka.
Kifo
kimetuondolea mpigania haki, kifo kimetupokonya jasiri wa karne ya 21, hakika Dk.
Magufuli anastahili kuliliwa milele.
Mimi Prudencia
Paul Kimiti ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Kudhibiti Uhalifu wa Ushuru wa
Forodha ndani ya Mamlaka ya Mapato na Kodi nchini Uingereza (HMRC),
sitaacha kumlilia.
Na ili kutimiza
ahadi yangu hiyo nimeiona haja ya kutuma Waraka wangu kwa Watanzania wenzangu.
Imani yangu ni
kuwa Waraka wangu huu utasalia kuwa kumbukumbu ya maombolezo yangu kwa Hayati
Dk. Magufuli na Tanzania kwa ujumla.
*POLE*
Nianze kwa
kuwashukuru Watanzania kwa mapenzi mkubwa waliyoyaonesha kwa nchi na kwa
Hayati Dk Magufuli.
Wamemuenzi
kishujaa na kuionesha dunia kuwa walikuwa na mapenzi ya kweli ya Dk. Magufuli
ambaye alipachikwa majina mengi ya kishujaa kama vile Bulldozer, Jembe na Jiwe.
Pili nachukua
nafasi hii adimu na adhimu kumpa pole Rais Samia Suluhu Hassan.
Wote tunakubali
kuwa kwa sasa tumo ndani ya kipindi kigumu kilichojaa majonzi na
maombolezo makubwa.
Aidha
nampa pole Mama Janeth Magufuli na familia yote ya hayati Dk. Magufuli,
ndugu, jamaa, marafiki na kwa Watanzania wote popote walipo duniani.
Kifo cha Dk. Magufuli
kimetuumiza wote, na tunapaswa kumwomba Mwenyezi Mungu azidishe Upendo
kwa Watanzania na hasa kwa mama yetu Rais Samia.
Tunamwomba awe
jasiri na shupavu katika kuendelea kuwapigania raia wake hasa wanyonge, kulinda
uhuru wetu, maslahi, haki na heshima yetu kama Taifa.
Tuna imani
kubwa kwamba chini ya uongozi wako imara na shupavu hatuwezi kuwa wapweke wala
wakiwa.
Imani hiyo hiyo
inatupa matumaini kuwa utaendelea kutimiza majukumu ya kuliongoza na
kulivusha taifa letu kwenye mambo yote yanayolikabili sasa na siku zijazo, kwenye raha na karaha.
Tunamuomba
Mwenyezi Mungu akulinde, udumu na kuendelea kulinda maslahi ya Watanzania
ambayo hayati Dk. Magufuli aliwapigania siku hadi siku.
Sisi tulio
ughaibuni, mioyo yetu inaungana nanyi nyumbani katika maombi, machumgu,
maumivu na huzuni.
Mola Atupe
faraja, subira na utulivu.
*RAI YANGU*
Rai yangu kwenu
viongozi, nawasihi kamwe msiache kuiga na kuyatafsiri maisha ya hayati Dk.
Magufuli.
Muenzini
kwa vitendo kwa kuendeleza yote aliyoyasimamia, kuukataa uzembe, kuikataa
rushwa, kuupinga ufisadi na kuwatetea wanyonge na kuipenda nchi yetu kwa
kuitakia mema.
Naamini hakuna
linaloshindikana, kama yeye aliweza basi nanyi mnaweza, mnaweza kwa sababu mliyaweza
hayo pamoja nae. Yaendelezeni.
*MAMA SAMIA
ANAWEZA*
Mama Samia ni kati
ya kinamama jasiri wanaoweza kuifikisha nchi mahali alipotarajia Hayati
Magufuli.
Uzoefu wa kazi
aliuonyesha akiwa Serikalini Zanzibar unatosha kuwa na imani nae.
Alipoteuliwa na
Wabunge wa Bunge la Katiba kumsaidia Marehemu Samuel Sitta, ilidhihirisha wazi
kuwa ni mwanamke shupavu na hodari.
Kuwa kwake
Makamu wa Rais wa shujaa na sauti ya wanyonge Hayati Dk. Magufuli kwa
kipindi cha miaka mitano na miezi minne kulitosha kunoa makali yake ya
kiuongozi.
Naamini ni Rais
mwenyewe kumuamini Mungu kama ilivyokuwa kwa mtangulizi wake.
Mama huyu
anafaa kuendeleza mapambano katika kipindi kingine cha pili.
Mama Samia ni
mpambanaji anajua mbinu zote za kivita kwenye mapambano haya ya kiuchumi.
Ni nahodha mwenye
uwezo wa kulifikisha salama jahazi hili la Tanzania.
Sisi watanzania
bila kujali tupo eneo gani la nchi hii tupo naye na tutamtakia kheri ili
alifikishe jahazi hili salama.
Poleni
Watanzania wenzangu, poleni Waafrika na pole kwa dunia.
Sote tunakiri
kuwa kifo hakina huruma na ndio maana imetuchukulia shujaa wetu Dk. John Joseph
Magufuli.
Mungu ailaze
roho ya mpendwa wetu Hayati Dk. John Magufuli mahali pema peponi. Amen.
Mungu
Ibariki Tanzania, Mungu Ibariki Afrika.

Post a Comment