Marekani yasema 'imefadhaishwa sana' na mswada wa Ghana dhidi ya wapenzi wa jinsia moja

 


Marekani imesema "imefadhaishwa sana" na kupitishwa nchini Ghana kwa sheria kali dhidi ya LGBTQ+, ambayo inasema inatishia uhuru wa kikatiba.

"Muswada huo pia utadhoofisha afya ya umma , vyombo vya habari na uhuru wa kiraia, na uchumi," msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani Matthew Miller alisema katika taarifa.

Imetoa wito wa "mapitio ya uhalali wa mswada".

Mswada mpya uliopitishwa Jumatano unatoa kifungo cha hadi miaka mitatu jela kwa yeyote atakayepatikana na hatia ya kujitambulisha kama LGBTQ+.Pia inaweka kifungo cha juu zaidi cha miaka mitano jela kwa kuunda au kufadhili vikundi vya LGBTQ+.

Kupitishwa kwa mswada huo kumekosolewa na mashirika ya haki na makundi mengine.

Rightify Ghana ilishutumu vikali "sheria hii ya ukandamizaji, ambayo inaleta tishio kubwa kwa haki na uhuru wa watu binafsi wa LGBTQ+ nchini".

Mkurugenzi mtendaji wa UNAIDS Winnie Byanyima alisema mswada huo, iwapo utakuwa sheria, unaweza kuchochea ghasia za Waghana dhidi ya raia wenzao.

Alisema kuwa "itazuia upatikanaji wa huduma za kuokoa maisha, kudhoofisha ulinzi wa kijamii, na kuhatarisha mafanikio ya maendeleo ya Ghana."

Mswada huo utawasilishwa kwa Rais Nana Akufo-Addo na baada ya hapo atakuwa na siku saba za kuutia saini kuwa sheria au kukataa kuupitisha, kwa mujibu wa katiba ya Ghana.

No comments