Korea Kaskazini yadai kufanikiwa kurusha satelaiti ya kijasusi baada ya kushindwa hapo awali

 


Korea Kaskazini inadai kuwa imefanikiwa kuweka satelaiti ya kijeshi ya kijasusi angani, baada ya majaribio mawili ya awali kufeli mwaka huu.

Hatua hiyo inajiri baada ya mkutano kati ya Rais wa Urusi Vladimir Putin na Kim Jong Un mnamo Septemba, ambapo Moscow ilitoa msaada wa Pyongyang katika mpango wake wa anga.Korea Kusini inasema bado haijathibitisha iwapo satelaiti hiyo inafanya kazi.

Lakini inasema inaamini Kaskazini ilipokea msaada kutoka kwa Urusi.Kufuatia uzinduzi huo, Korea Kusini ilitangaza kuanza tena ufuatiliaji katika mpaka wake na Kaskazini, na hivyo kuchukua hatua za kusimamisha sehemu za makubaliano yaliyokubaliwa na nchi hizo mbili mnamo 2018 yenye lengo la kupunguza mvutano wa kijeshi.

Shirika la habari la serikali ya Korea Kaskazini KCNA limesema satelaiti hiyo inayoitwa Malligyong-1, iliingia "kwa usahihi" kwenye obiti na kiongozi Kim Jong Un aliona kurushwa kwake.

Uzinduzi huo umelaaniwa na Umoja wa Mataifa, ambao unashikilia vikwazo kwa Korea Kaskazini kutokana na uundaji wake wa makombora ya nyuklia, na nchi zingine zikiwemo Marekani na Japan.Katibu

Mkuu wa Umoja wa Mataifa alisema: "Urushaji wowote unaofanywa na [Korea Kaskazini] kwa kutumia teknolojia ya makombora ya balestiki ni kinyume na maazimio husika ya Baraza la Usalama."Alisisitiza wito kwa Kaskazini kurejea katika njia yake ya kuondoa nyuklia.

Ikulu ya White House imesema hatua hiyo ni "ukiukaji mkubwa" wa maazimio ya Umoja wa Mataifa, wakati waziri mkuu wa Japan, Fumio Kishida, pia alikashifu uzinduzi huo - ambapo roketi ya setlaiti hiyo iliruka juu ya mkoa wa Okinawa nchini humo na kuelekea Bahari ya Pasifiki.

Serikali ya Japani ilitoa onyo la dharura kwa muda mfupi, ikiwaambia wakazi wa Okinawa wajihifadhi. Korea Kaskazini iliiambia Japan siku ya Jumatatu kuwa inakusudia kujaribu kurusha tena satelaiti yake.

Ilikuwa imejaribu mara mbili mwaka huu na ikashindwa - Mei na Agosti.Bw Kishida alilaani uzinduzi huo "kwa maneno makali" na kusema malalamiko yamewasilishwa kwa Korea Kaskazini.

"Hata ikiwa lengo ni kurusha satelaiti, kutumia teknolojia ya makombora ya balestiki ni ukiukaji wa wazi wa maazimio husika ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa," alisema Bw Kishida.

No comments