BASHUNGWA AAGIZA TATHIMINI UJENZI WA MIZANI
Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa, ameagiza wataalam wa wizara hiyo kufanya tathimini ya mizani zote nchini na kuangalia bajeti ya kuweka mizani ya kigitali ya kupima uzito wa magari yakiwa kwenye mwendo (weigh in motion), ili iwe katika vipaumbele vya Serikali katika mizani zote ambazo hazijafungwa mfumo huo na zile zitakazojengwa.
Bashungwa ameyasema
hayo Oktoba 3, 2023 mkoani Mbeya wakati akikagua kazi zinazoendelea katika
mzani wa Uyole uliopo mwanzoni mwa barabara ya Uyole - Kasumulu (mpakani mwa
Tanzania na Malawi).
"Dhamira ya
Serikali ya kujenga mizani hizi nchini sio kutoza tozo bali ni kujenga
utamaduni wa kutozidisha uzito ili kulinda barabara zetu", amesema
Bashungwa.
Ameongeza kuwa Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu ametoa fedha ya
ujenzi wa njia nne wa barabara ya Nsalaga – Ifisi (km 29), ili kupunguza foleni
katika barabara hiyo hivyo ni vema na mizani zitakazokuwepo ziendane na
barabara hiyo.
Aidha, Bashungwa ametoa
wito wa wasafirishaji wote nchini kuendelea kuzingatia viwango vya uzito
vilivyotolewa kwa ajili ya kutumia barabara zetu ili kuendelea kuzilinda
barabara na kuepuka kuingia gharama za tozo za kuzidisha uzito.
Naye, Mkurugenzi wa Miradi kutoka Wakala wa Barabara Tanzania
(TANROADS), Eng. Boniface Mkumbo amesema mzani huo unasaidia kudhibiti
magari ya mizigo na ya abiria yanaoenda /yanaotoka Malawi, Kyela na Rungwe.

.jpg)

Post a Comment