SERIKALI YASEMA SEKTA YA MIUNDOMBINU YABORESHWA MIAKA 60 YA UHURU

 

 

 

Serikali imesema inaendelea kutekeleza na kuboresha miundombinu nchini kupitia Sekta ya Ujenzi na Uchukuzi kwa kuhakikisha kuwa huduma za usafiri na usafirishaji zinakuwa nafuu na uhakika katika maeneo mbalimbali nchini.

Hayo yamesemwa leo Jijini Dodoma na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu hatua mbalimbali za ukuaji wa sekta hizo tangu kipindi cha uhuru wa Tanzania Bara hadi sasa.

“Katika kipindi cha miaka ya Uhuru wa Tanzania Bara (1961-2021), Serikali imepata mafanikio makubwa kupitia Sekta hizi mbili, aidha kumekuwa na mabadiliko mbalilmbali ya kisera yaliyoendana na utungwaji wa sheria kadhaa zilizowezesha sekta hizi kuendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, amesema Prof. Mbarawa”.

Mbarawa ametaja mafanikio yaliyopatikana kupitia Sekta hizo kuwa ni pamoja na Ongezeko la mtandao wa barabara za lami kutoka 1,360 mwaka 1961 hadi kufikia kilometa 11,186, Septemba 2021  na hivyo kurahisisha huduma za usafiri na usafirishaji katika maeneo mbalimbali nchini.

Ameongeza kuwa katika kipindi cha miaka 60 ya Uhuru, Serikali pia imejenga madaraja makubwa na madogo yakiwemo Daraja la Mto Kagera, Daraja la Rusumo, Mkapa, Umoja, Kikwete, Sibiti, Mara, Mlalakuwa na Daraja la Momba.

Ametaja madaraja mengine kuwa ni Lukuledi II, Ruhuhu, Magufuli, Magara, Nyerere, Kavuu na Ruvu Chini na kuongeza kuwa baadhi ya madaraja makubwa yanayoendelea ni pamoja na Daraja la Tanzanite, Msingi, Wami, Gerezani na Kigongo- Busisi.

Aidha, Waziri Mbarawa amefafanua kuwa Serikali inaendelea na mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa yenye upana wa mita 1.435  Standard Gauge Railway – SGR ambapo amesema kuwa Awamu ya Kwanza ya mradi huo ni ya ujenzi wa reli ya kutoka  Dar es salaam hadi Mwanza kilomita1,219 ambayo imegawanyika katika vipande vitano ikiwemo kipande cha kutoka Dar essalam hadi Morogoro kilomita 300,  kipande cha Morogoro Makutupora kilomita 422,  kipande cha Makutupora Tabora kilomita 376.5  kipande cha Tabora Isaka kilomita 162.5 na kipande cha Isaka Mwanza kilomita 341.

Amebainisha lkuwa Serikali inatambua umuhimu wa usafiri wa anga katika kuchangia ukuaji wa sekta nyingine hasa utalii wa aina zote kilimo cha mbogamboga , matunda nyama na samaki na kuinua uchumi wa nchi na ustawi wa wananchi.

Waziri Profesa Makame Mbarawa leo ametoa Taarifa ya Wizara yake kuhusu utekelezaji wa miradi, mafanikio na changamoto kwa waandishi wa habari jijini Dodoma katika kipindi cha miaka 60 ya Uhuru hadi sasa.

 

 

 

No comments