SERIKALI YASEMA SEKTA YA MIUNDOMBINU YABORESHWA MIAKA 60 YA UHURU
Serikali imesema inaendelea kutekeleza na kuboresha
miundombinu nchini kupitia Sekta ya Ujenzi na Uchukuzi kwa kuhakikisha kuwa huduma
za usafiri na usafirishaji zinakuwa nafuu na uhakika katika maeneo mbalimbali nchini.
Hayo yamesemwa leo Jijini Dodoma na Waziri wa Ujenzi
na Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu
hatua mbalimbali za ukuaji wa sekta hizo tangu kipindi cha uhuru wa Tanzania Bara
hadi sasa.
“Katika kipindi cha miaka ya Uhuru wa Tanzania Bara
(1961-2021), Serikali imepata mafanikio makubwa kupitia Sekta hizi mbili, aidha
kumekuwa na mabadiliko mbalilmbali ya kisera yaliyoendana na utungwaji wa sheria
kadhaa zilizowezesha sekta hizi kuendelea kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi,
amesema Prof. Mbarawa”.
Mbarawa ametaja mafanikio yaliyopatikana kupitia Sekta
hizo kuwa ni pamoja na Ongezeko la mtandao wa barabara za lami kutoka 1,360
mwaka 1961 hadi kufikia kilometa 11,186, Septemba 2021 na hivyo kurahisisha huduma za usafiri na usafirishaji
katika maeneo mbalimbali nchini.
Ameongeza kuwa katika kipindi cha miaka 60 ya Uhuru,
Serikali pia imejenga madaraja makubwa na madogo yakiwemo Daraja la Mto Kagera,
Daraja la Rusumo, Mkapa, Umoja, Kikwete, Sibiti, Mara, Mlalakuwa na Daraja la
Momba.
Ametaja madaraja mengine kuwa ni Lukuledi II,
Ruhuhu, Magufuli, Magara, Nyerere, Kavuu na Ruvu Chini na kuongeza kuwa baadhi ya
madaraja makubwa yanayoendelea ni pamoja na Daraja la Tanzanite, Msingi, Wami,
Gerezani na Kigongo- Busisi.
Aidha, Waziri Mbarawa amefafanua kuwa Serikali inaendelea
na mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa yenye upana wa mita 1.435 Standard Gauge Railway – SGR ambapo amesema kuwa
Awamu ya Kwanza ya mradi huo ni ya ujenzi wa reli ya kutoka Dar es salaam hadi Mwanza kilomita1,219
ambayo imegawanyika katika vipande vitano ikiwemo kipande cha kutoka Dar
essalam hadi Morogoro kilomita 300,
kipande cha Morogoro Makutupora kilomita 422, kipande cha Makutupora Tabora kilomita
376.5 kipande cha Tabora Isaka kilomita
162.5 na kipande cha Isaka Mwanza kilomita 341.
Amebainisha lkuwa Serikali inatambua umuhimu wa usafiri
wa anga katika kuchangia ukuaji wa sekta nyingine hasa utalii wa aina zote kilimo
cha mbogamboga , matunda nyama na samaki na kuinua uchumi wa nchi na ustawi wa wananchi.
Waziri Profesa Makame Mbarawa leo ametoa Taarifa ya
Wizara yake kuhusu utekelezaji wa miradi, mafanikio na changamoto kwa waandishi
wa habari jijini Dodoma katika kipindi cha miaka 60 ya Uhuru
hadi sasa.

Post a Comment