USHIRIKINA NI SEHEMU YA MAISHA YA WASWAHILI


The Best Movies About Ghosts | IndieWire

MAISHA yana sarakasi nyingi sana. Zipo simulizi za kila aina zinazosimulia jinsi baadhi yetu tunavyoishi katika dunia ya giza. Kuna watu wanakimbia makwao kule vijijini wakiogopa uchawi na wapo ambao hawataki kabisa kurudi huko wakiogopa ushirikina.

Utafikiri labda huku mijini wanakoishi hakuna wachawi au na wao hawajishughulishi nao. Mijini ndipo kwenye waganga wengi zaidi, na waswahili wanapishana kwenye milango yao wakitaka huduma.

Huyu anataka dawa ya kinga, akidai majirani wanamuonea kijicho, huyu atasema anataka kumfunga mume wa mtu maana mkewe anambana sana, yule atataka dawa ya kuwa karibu na bosi ofisini kwake, mwingine atataka afanyiwe mpango amng'oe kitini mwenzake.

Mtu atafungua kajibiashara kake labda cha kupika maandazi, chapati au kuchoma mihogo, lakini lazima aende kwanza kwa babu, apewe vimitimiti avitafune ndipo aridhike kwamba sasa anaweza kuendelea na shughuli. Kwa nini, ana hofu kwamba kwa kuwa watu hatutakiani mema, basi lazima tu kuna mtu atamtia nuksi.

Hatuna ushahidi, lakini namna tunavyoendesha maisha yetu, ni dhahiri kuwa mtu anaweza kwenda 'kumshughulikia' mwenzake kwa mganga ili mradi tu amkwamishe mishe mishe zake. Tena huyo aweza kuwa mtu wake wa karibu kabisa, kila siku akimpelekea shida zake. Lakini anataka amkwamishe maana anamuona kama anajidai.

Badala ukamshughulikie ili Mungu azidi kumbariki apate kukusaidia zaidi, eti unataka na yeye akwame, sasa shida zako utazimalizia wapi?

Watu wanaishi wanakuambia wanamuomba Mungu tu, ndiye kimbilio lao. Waongo wakubwa...kama kuna watu wanaojidanganya wenyewe, basi ni wale wanatudanganya kwa kukaa sana kwenye nyumba za ibada na kushiriki kila sala. Iwe waislamu au wakristo. Kwa utafiti wangu, hawa ndiyo wanaongoza kwa kumiliki hirizi na kufanya makafara majumbani mwao.

Unamuona mtu swala tano kwa ndugu zangu waislamu, lakini kila siku anafanya matambiko nyumbani kwake, kila siku yupo kwa mtabiri na mganga wa vitabu. Basi bora hayo anafanya kwa kificho, lakini swala tano huyu kila akikaa sehemu, kazi yake ni kusengenya wenzake, huyu ana hivi, huyu ana vile. Mcha Mungu gani wewe?

Njoo kwa ndugu zangu wakristo. Hakosi ibada, iwe wa Jumuia, Jumapili au Hija. Muda wote utamuona na bibilia yake mkononi, rozari shingoni na sebuleni kwake mabango ya Yesu yamesheheni. Lakini nyuma ya pazia, ana hirizi.

Ni kweli anamuamini Mungu, lakini anawaogopa wanadamu. Anajikinga, maana wanasema jisaidie ili usaidiwe.

Mtu haanzi kujenga nyumba yake bila kumwaga ungaunga au kufanya kisomo kinachoambatana na uchinjaji wa kuku au mbuzi. Mtu akipita nyumbani kwake mara mbili au tatu ameshaanza kumtilia shaka, siyo kwamba ni mwizi, la. Mama au baba mtu mzima ataiba nini hapa, huyu kuna kitu anataka kufanya!

Maisha yetu yametawaliwa sana na imani hizi. Hata wenzetu waliofanikiwa kimaisha, bado hatuwaamini, tunaona kama kuna giza nyuma ya utajiri wao. Utawasikia tu wanasema, yule mganga wake namjua, aliuaga ndugu zake!

Jamani, kwani mtu ukifanikiwa ndiyo ndugu zako wasife na wakifa eti umewaua wewe? Hebu huyo anayesema aliyefanikiwa ameua ndugu zake, je yeye hana ndugu aliyekufa?

Kitu cha msingi na ambacho ningependa nikuache nacho. Ni juu yako kuamua, uufuate ushirikina au uuache. Vyovyote utakavyoamua, huna lolote utakalobadili kama hautafanya jitihada za kutimiza lile ulilolipanga kwa kufuata kanuni zilizopo maana maisha yetu yote yametawaliwa na kanuni.

 

No comments