MELI ILIYOZIBA MFEREJI WA SUEZ YAINGIZA HASARA YA MAMILIONI KILA SIKU

Inakadiriwa kuwa kuna
hasara ya dola milioni nne kwa saa baada ya meli kubwa ya kontena kuziba
Mfereji wa Maji wa Suez nchini Misri. Mfereji huo ni kati ya njia zenye
shughuli nyingi zaidi za meli za kibiashara duniani.
Kwa mujibu wa
makadirio ya Shirika la Lloyd List, baada ya meli hiyo kuziba Mfereji wa Suez,
meli zilizokwama kuelekea upande wa maghairbi zinapata hasara ya dola bilioni
5.1 kwa siku na zile zilizokwama upande uneoelekea mashariki zinapata hasara ya
takribani dola bilioni 4.5 kwa siku.
Kwa mujibu wa data
zilizokusanywa na Shirika la Habari la Bloomberg, hivi sasa kuna jumla ya meli
185 ambazo zinasubiri kupita Mfereji wa Suez. Miongoni mwa meli hizo kuna meli
27 kubwa za mafuta ambazo zina takribani mapipa milioni 1.9 ya mafuta ghafi ya
petroli.
Meli iliyoziba
Mfereji wa Suez ina urefu wa mita 400 sawa na viwanja vinne vya mpira wa miguu
na imekwama kwenye mfereji wa Suez unaounganisha Bahari ya Mediterania na
Bahari ya Sham na hivyo kuzuia meli kupita huku shughuli mbalimbali muhimu
zikivurugwa. Kukwama kwa meli hiyo kumesababisha bei ya mafuta kupanda kwenye
masoko ya kimataifa.
Karibu asilimia 12
ya biashara ulimwenguni hupita katika mfereji wa Suez na ni njia ya mkato kati
ya Bara la Asia na Ulaya. Meli hiyo iliyosajiliwa nchini Panama na kuendeshwa
na kampuni ya usafirishaji ya Evergreen, ilikuwa ikielekea bandari ya Rotterdam
nchini Uholanzi ikitokea China na ilikuwa ikipita Kaskazini kupitia mfereji huo
kuelekea Mediterranean. Meli hiyo ya tani 200,000 ilitengenezwa mwaka 2018.
Juhudi za kuikwamua
meli hiyo zingali zinaendelea huku wakuu wa Misri wakisema huenda zoezi hilo
likachukua siku kadhaa.
Meli ambazo
haziwezi kusubiri zitalazimika kuzunguka bara Afrika ili kufika Ulaya na hivyo
kurefusha safari kwa takribani wiki mbili zaidi.

Post a Comment